Msafiri Diouf:

Ama kweli dawa za kulevya ni hatari

Msafiri Diouf ameamua kutoa ya moyoni na kudai wasanii wengi nchini wamekuwa wakitumia dawa za kulevya kitu ambacho kinasababisha kupoteza mwelekeo na hata kupoteza maisha.




Diouf ambaye alikiri kutumia madawa hayo toka mwaka 1996 alisema alikata shauri mwenyewe na kwenda kutibiwa kwenye hospitali ya Lutindi iliyopo Wilaya ya Korogwe mkoani Tanga.

“Nilianza kubwia unga toka mwaka 1996, sikujua kama unga una madhara, awali nilikuwa navuta bangi lakini kuna jamaa mmoja sasa hivi ni marehemu ndio alinifundisha kubwia unga.”

“Kuna wakati alikuwa anachanganya unga na bangi. hata hivyo mimi na wenzangu hatukujua kama anachanganya na bangi, kuna siku akatupa bangi bila ya kuchanganya na unga tulivyovuta tukaona mbona ipo tofauti na haileti ulevi sana, tukamuliza hii vipi mbona mbaya akasema sijawachanganyia, tukamuuliza hujatuchanganyia na nini akasema unga, tukamwambia tuchanganyie basi, kweli alipochanganya tukavuta tukajiona kama tuko Ulaya vile, dunia yote ipo mikononi mwako.”

“Kuanzia hapo ndio nikafungua ukurasa mpya wa kutumia dawa za kulenya, nikafikia kipindi nikaacha kuchanganya na bangi, nikawa nabwia na kunusa, wakati ule kete moja ilikuwa ikiuzwa Sh250 sasa hivi inauzwa Sh2,000.”

“Uteja ni kitu ambacho kinaweza kukudhoofisha, mimi ulikuwa ukinidhoofisha kwani nilikuwa siwezi kupanda stejini kuimba kama sijabwia, nilikuwa mteja msafi, kipindi cha mwazo watu walikuwa hawajui kama mimi ni teja, ila wale wa karibu wakawa wananiambia mbona sauti inabadilika kama inakwaruza na kukauka.”

“Ilifika wakati mwili ulidhoofu, Diofu wa leo sio yule sasa hivi nina afya hata wewe si unacheki, nilikonda sana nilifikia hatua nikawa nikilala saa 10 usiku tunapomaliza kuimba siamki mpaka saa moja usiku, na nikiamka nakula kisha lazima nibwie ndio nitajisikie freshi.

ILIKUWAJE AKAACHA:

“Unajua mwanzoni mke wangu na ndugu zangu walikuwa wakinikamata kwa nguvu na kunipeleka hospitali, basi nikajikuta naacha na kurudia, sikuwahi kuacha moja kwa moja kama ilivyo sasa.”

“Nina watoto wawili, Najma a.k.a Vannesa na Taslim a.k.a Paris’ sasa roho iliniuma sana siku moja watoto wenzao walikuwa wanawaambia baba yenu nyie ni teja.

“Nilijisikia vibaya kuona watoto wangu watazidi kusakamwa kwa kuambiwa kuwa baba yao (mimi)ni teja.
“Hali hiyo ndio iliyonifanya niamue kukata shauri na kwenda Muhimbili nikaonana na Dokta Ayubu ambaye yeye akanipeleka Lutindi, hiyo ilikuwa ni mwaka jana na nilikaa hospitali kwa miezi mitatu lakini toka nimetoka huko nina miezi tisa na bado naendelea kupata ushauri Muhimbili, huwa naenda kila Jumatano na Ijumaa.”

WASANII KUPOTEZA MAISHA KWA AJILIYA UNGA

“Wasanii wengi wanatumia dawa za kulevya, wengi nimewaona wamedhoofika, namshukuru Mungu kwa kunitoa katika janga hilo.”

0 comments:

Post a Comment