WANAUME SITA WALIOMBAKA MTALII WA USWISI WAFUNGWA MAISHA JELA...

Mahakama ya India juzi imewahukumu kifungo cha maisha jela wanaume sita waliopatikana na hatia ya kumbaka mwanamke raia wa Uswisi, katika moja kati ya kesi kadhaa za hivi karibuni ambazo zimechochea maandamano ya kulaani ongezeko kubwa la matukio ya ubakaji nchini India.

Mwanamke huyo kutoka Uswisi mwenye miaka 39 alibakwa wakati akiwa amepiga kambi na mumewe kwenye msitu katikati ya jimbo la Mandya Pradesh nchini India katikati ya mwezi Machi.
"Ilikuwa hukumu nzuri. Imekutolewa mapema," alisema Rajendra Tiwari, mwanasheria wa serikali.
Mwanamke huyo hapo kabla aliwataka majaji kujaribu kutowapa washambulizi wake sita hukumu ya kifo.
Majaji mjini Daita, katikati ya India, walianza kesi na wanne kati ya sita waliotuhumiwa kwa kubaka na wengine wawili wanakabiliwa na mashitaka ya kushambulia na ujambazi.
Mahakama ilielezwa kwamba muathirika huyo mwenye miaka 39 na mumewe walikuwa wakisafiri kwa kutumia baiskeli wakati walipokuwa mapumzikoni katika jimbo la Mandya Pradesh ndipo kambi yao iliposhambuliwa na kundi hilo.
Baada ya kumpiga na kumfunga kamba mumewe mwenye miaka 30, kundi hilo lilimwangusha na kumbaka mkewe aliyekuwa amejawa na hofu, walisema waendesha mashitaka.
Baraza la Taifa la Kumbukumbu za Uhalifu linasema zaidi ya matukio 24,200 ya ubakaji yaliripotiwa kote nchini India mwaka 2011 - takribani moja katika kila dakika 20. Polisi wanakadiria matukio manne tu kati ya kumi yanaripotiwa, zaidi ni kutokana na hofu ya waathirika kuaibishwa na familia zao na jamii.
India imeshuhudia anguko kubwa la idadi ya watalii wa kigeni, hususani wanawake, tangu tukio kubwa na baya zaidi la ubakaji na mauaji ya msichana mjini New Delhi, Desemba mwaka jana.
Katika miezi mitatu tangu shambulio lile, idadi ya wageni wanaosafiri kwenda India imeshuka kwa asilimia 25, kwa mujibu wa ripoti.
Idadi ya watalii wa kike imeshuka kwa asilimia 35, utafiti uliotolewa hadharani juzi ulisema.
Utafiti huo ulitembelea watu 1,200 wanaohudumia watalii kutoka kote nchini humo ambao walisema 'suala la usalama wa wasafiri wa kike' limechangia jinsi wasafiri wa kigeni wanavyotazamwa nchini India.
Tangu tukio la ubakaji la Desemba kumekuwa na matukio yaliyotangazwa mno ambako wasafiri wa kike wa kigeni wameshambuliwa.

0 comments:

Post a Comment