Viongozi watekwa, wamwagiwa upupu


VIONGOZI wa Chama cha Msingi cha Ushirika wa Mazao na Masoko Lenganelo na Diwani wa Mchemo, Mshamu Chituta, wamekamatwa na wanachama, wakafungiwa katika ghala la korosho na kumwagiwa upupu.
Akizungumzia kisa hicho katika Baraza la Madiwani juzi, diwani huyo alisema wanachama hao walishikwa na hasira mkutanoni, baada ya kudanganywa, ndipo walipomkamata yeye na uongozi wa chama hicho na kuwafungia kisha kuwamwagia upupu.
Alitaja wenzake waliopata adhabu hiyo kuwa ni Mwenyekiti wa Chama hicho, Hassan Nakuya, Katibu aliyemkumbuka kwa jina moja la Mnali na msaidizi wake, Ramadhani Mpanga. Chituta alisema uongozi wa chama hicho, ulitangazia wananchi kwenye mkutano huo, kuwa Mkuu wa Wilaya ya Newala, Christopher Magalla, angekuwapo.
Habari kutoka eneo la tukio, zilieleza kuwa viongozi wa chama hicho walitumia jina la Mkuu wa Wilaya kuitisha mkutano wa wanachama, ili kuwavuta wahudhurie kwa wingi. Diwani Mshamu alisema hakuwa anajua kama uongo ulitumika, kwa kuwa siku ya tukio alikuwa na kikao cha Kamati ya Maendeleo ya Kata, lakini aliombwa na Katibu wa Chama cha msingi, asitishe kikao hicho na aende kwenye mkutano wa chama ambao pia ungehudhuriwa na Mkuu wa Wilaya.
Kwa mujibu wa diwani huyo, wanachama waliitika mwito lakini mkutano ulianza bila Mkuu wa Wilaya, wakagundua kudanganywa ndipo wakaamua kuwaadhibu viongozi na yeye kwa kuwafungia ghalani na kuwamwagia upupu.
Alisema walijaribu kuwasiliana na Mkuu wa Wilaya, ili afike kuwanusuru, lakini simu yake haikupatikana hivyo wakakaa ghalani kwa saa kadhaa, mpaka walipomtafuta Mkuu wa Polisi wa Wilaya (OCD), aliyefika kuwafungulia.
Kutokana na malalamiko hayo ya diwani katika Baraza hilo ambalo Magalla pia alihudhuria, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Newala, Ashidi Ndembo, alimwomba Mkuu wa Wilaya, kutoa ufafanuzi wa suala hilo, ili kuondoa hali ya sintofahamu baina ya diwani na uongozi wa chama cha msingi. Majibu ya DC Akijibu hoja hizo, Magalla alisema hakuwa na taarifa na mkutano huo na kwamba siku inayotajwa kufanyika mkutano huo, alikuwa kwenye kikao cha Kamati ya Ulinzi na Usalama cha Mkoa mjini Mtwara.
“Nataka nichukue nafasi hii kueleza kwamba sikuwa na taarifa ya mkutano huo, siku hiyo nilikuwa katika kikao mjini Mtwara na simu nilizima kutwa nzima. Nilipoiwasha, nilikuta ujumbe kutoka kwa mtu nisiyemjua, nilipopiga simu nikagundua ni Mwenyekiti wa Chama cha Msingi cha Lenganelo,” alisema Magalla.
Alisema baada ya kumpigia, Mwenyekiti huyo alimfahamisha kuwa alikuwa amefungiwa ghalani na wakulima na alimpigia kutaka msaada lakini simu haikupokewa, ingawa walishafunguliwa. Magalla alionya wanaotumia jina lake kuitisha mikutano ya wananchi kwa kuwa kitendo hicho ni kinyume cha sheria na utovu wa nidhamu, alitaka wahusika wa jambo hilo waache kabla hatua za kisheria hazijachukuliwa dhidi yao.
“Nimesikitishwa sana na kitendo hiki, hasa ninaposikia kinafanywa na viongozi wenzangu. Kwa kweli si jambo jema…tunajua kuna baadhi ya maeneo wananchi wamekuwa hawajitokezi wanapoitwa katika vikao na mikutano, sasa kama viongozi wa eneo hilo wanahitaji msaada wa DC, ni vema wakawasiliana nami na kwa kuwa huo ni wajibu wangu nitakuja,” alisema Magalla.
chanzo-habari leo

0 comments:

Post a Comment